Wabunge waliosusa wazidi kubanwa



WABUNGE wa kambi ya upinzani waliosusa vikao vya Bunge, vinavyoendeshwa na Naibu Spika, Tulia Ackson, wameendelea kubanwa, wakiambiwa kuendelea kufanya hivyo ni kutofahamu wajibu wao wa uwakilishi kwa wananchi.
Watu wa kada mbalimbali wakiwemo viongozi wa dini, wa vyama vya siasa na baadhi ya wabunge wa CCM, wamewataka hao wenzao waliosusa, kutengua msimamo wao, warudi bungeni kuleta afya katika mijadala.
Miongoni mwa waliozungumzia hilo ni Mbunge wa Mtera (CCM), Livingostone Lusinde, aliyesema wapo baadhi ya wabunge wa upinzani, wamemhakikishia kuwa wako tayari kuingia bungeni lakini wanashindwa kufanya hivyo kwa kuzuiwa na Kiongozi wa kambi hiyo bungeni, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taifa wa Chadema, Freeman Mbowe.
Askofu awashangaa
Askofu wa Kanisa la Methodist Tanzania Jimbo la Dodoma, Joseph Bundala alisema kitendo wanachofanya wabunge hao wa upinzani ni kutojua wajibu wao kama wawakilishi wa wananchi.
Akihubiri kwenye ibada ya Jumapili iliyopita katika kanisa hilo ililopo Ipagala Manispaa ya Dodoma, askofu huyo alisema wanadhihirisha kuwa wachanga kidemokrasia.
Askofu Bundala alisema, kususia vikao vya Bunge vinavyoongozwa na Naibu Spika, Dk Tulia hakuna maana bali wanachotakiwa kufahamu ni kwamba, wanapaswa kuchangia mijadala kwa ajili ya wananchi waliowachagua.
“Kama kiongozi wa dini, nawasihi wabadilike haraka kutoka katika hali ya uchanga na kufikiria utimilifu wa kidemokrasia,” alisema na kusisitiza kuwa kufanya hivyo, watatenda haki kwa wananchi waliowatuma. Wakati huo huo aliwataka kuacha kulisema vibaya Jeshi la Polisi, lenye jukumu la kulinda amani na utulivu. Alisisitiza hakuna nchi isiyoongozwa na sheria.
Lusinde awavaa
Kwa upande wake, Mbunge wa Mtera, Livingostone Lusinde (CCM) alisema wabunge wengi wa upinzani wamemhakikishia kuwa wako tayari kuingia bungeni lakini wanashindwa kufanya hivyo kwa sababu wanazuiwa na kiongozi wa kambi hiyo ya upinzani, Mbowe.
“Wako hapo kwenye chai, wamenituma nije niwasemee kwamba wako tayari kuingia bungeni lakini Mbowe anawapigia simu na kuwazuia wasiingie. Hata hivi ninavyoongea watakuwa wananipigia makofi kwa kuwasemea,” alisema Lusinde bungeni jana.
Akichangia Bejeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2016/15 na hali ya uchumi kwa mwaka 2015, Lusinde alimshauri Mbowe kuacha udikteta ili wabunge hao watoe mchango wao katika mjadala wa bajeti unaoendelea.
Hata hivyo, alisema kwa vile CCM ndicho chama mama, ni vyema wabunge wa chama hicho wakajadili hata kero za majimbo yanayoongozwa na ya wapinzani bila kubagua kwa faida ya Watanzania wanaoishi katika majimbo hayo.
Aliitaka serikali isiruhusu wapinzani kuendeleza siasa hata baada ya kampeni kumalizika kwa sababu wanasababisha vurugu katika kipindi ambacho serikali ina mambo mengi ya kufanya kwa ajili ya kuwapatia wananchi maendeleo.
“Kwa mfano, kama Mbowe analalamika kuhusu mambo yaliyotokea bungeni kwa nini asiende kwenye jimbo lake la Hai na badala yake anataka kwenda Kahama kwa Mheshimiwa Jumanne Kishimba. Hii ni fujo,” alisema na kuvitaka vyombo vya dola visiruhusu watu wasiopenda utulivu kwa sababu nchi haiwezi kuwa mwaka mzima inaendesha siasa za majukwaani.
Akigusia hoja hiyo wakati akijadili bajeti, Mbunge wa Kasulu mjini (CCM), Daniel Nsanzugwanko alishauri uongozi wa Bunge na wabunge wa CCM, watafute mwafaka kwa kuwasamehe wabunge wa upinzani ili warudi bungeni.
“Sisi (CCM) ni chama kikubwa na hatufaidiki na huu mgomo wa wapinzani. Tuwasamehe, tuwahurumie ili kumaliza hii stalemate (mgogoro),” alisema.
Hata hivyo, wakati akiahirisha shughuli za Bunge jana mchana, Naibu Spika, Dk Tulia Ackson alimjibu Nsanzugwanko kwamba hakuna aliyewatoa bungeni wapinzani na wala hawajakosa lolote kuhitaji kusamehewa, isipokuwa wanatoka nje kwa utashi wao.
Alirudia kusema kwamba kanuni zimeweka utaratibu mzuri wa nini cha kufanya, pale mbunge anapokuwa hakubaliani na uamuzi wa kiti kwa kuandika barua inayopelekwa kwenye kamati ya uongozi, jambo ambalo hawajafanya.
Mapema, wabunge wengi wa CCM waliochangia jana, walianza kwa kusifia utendaji wa Dk Tulia na kumtia moyo kwamba anaendesha vikao kwa weledi na hawajaona kosa alilofanya.
‘Rudini bungeni’
Wakati huo huo, akizungumza jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Taifa wa TLP, Augustino Mrema ametaka wabunge wa vyama vya upinzani, waliosusia vikao kurudi bungeni. Aliwataka warudi bungeni na kufuata demokrasia, badala ya kuachia mijadala yenye maslahi ya taifa ikiendelea kujadiliwa wenyewe wakiwa nje ya Bunge.
Alisema kitendo cha kumkataa Naibu Spika Dk Tulia na kutoka nje wakati akiwepo, hakifai kwa kuwa wanashindwa kuwawakilisha wananchi wao waliowatuma.
“Kama hawamtaki Dk Tulia wangetumia demokrasia, sasa watatoka nje hadi lini? Mi nawasihi warudi bungeni wafuate sheria, kanuni na taratibu,” alisema.
Kiongozi huyo wa TLP alisema yeye ni mpinzani, lakini ni msema kweli ambaye ataendelea kuwasema wasiotenda na kufuata haki na ambao ni mafisadi.
Alisema baadhi ya wapinzani, siyo wa kweli na wamekuwa wakilalamikia demokrasia kuvunjwa huku akiwashutumu kuwa wao wamekubuhu katika kuvunja haki za binadamu, sheria, katiba na demokrasia.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mrema alisema hali hiyo ndiyo ilifanya upinzani kushindwa katika majimbo mengi, waliyokuwa wakiyaongoza katika uchaguzi mkuu uliofanyika Oktoba mwaka jana.
“Baadhi ya wapinzani siyo wakweli kabisa kama wanavyosema na wananchi wanapaswa wawaelewe na wawe macho na kuwa makini na wanayowaambia. Kwa sababu wamekuwa wakidai haki lakini siyo wanayowafanyia wengine,” alisema.
Aidha Mrema aliwashutumu wapinzani kudai kwamba Rais Magufuli anaendesha serikali bila kuzingatia haki za binadamu, hawatendei haki, anavunja sheria na katiba, anawaonea na anaua demokrasia nchini.
“Wenyewe ndiyo vinara waliokubuhu kwenye vitendo hivyo kufanya hayo. Huu ni unafiki mkubwa na wananchi wawe makini na wapinzani wa namna hiyo,” alisema kiongozi huyo wa chama cha upinzani
Previous
Next Post »