Samatta afurahia kushindania tuzo ya Afrika

Mwanasoka wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta anayechezea KRC Genk ya Ubelgiji amesema kwamba kuingizwa kwenye kinyang'aniyo cha tuzo ya Mwanasoka Bora Afrika ni heshima kuu kwa nchi yake.
Samatta, kupitia wakala wake Jamal Kisongo, amesema amefurahi sana juu ya uteuzi huo, kwani anajiona anaendelea kuiwakilisha vyema nchi yake katika soka.
Mwanasoka Bora wa Afrika pamoja na kipa Mganda, Dennis Onyango anayechezea Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini na kiungo Mkenya, Victor Wanyama anayechezea Tottenham Hotspur ya England.
Orodha hiyo ina Waalgeria watatu; mshambuliaji wa mabingwa wa England, Riyad Mahrez, Islam Slimani wa Leicester City na El Arabi Hillel Soudani wa Dinamo Zagreb.
Mkongwe Samuel Eto'o anayechezea Antalyaspor ya Uturuki naye yumo kwenye orodha, pamoja na Mcameroon mwenzake, Benjamin Mounkandjo wa Lorient.
Wamo pia Pierre-Emerick Aubameyang (Gabon na Dortmund), Andre Ayew (Ghana na West Ham), William Jebor (Liberia na Wydad Athletic Club), Mehdi Benatia (Morocco na Juventus), Hakim Ziyech (Morocco na Ajax), John Mikel Obi (Nigeria na Chelsea), Kelechi Iheanacho (Nigeria na Manchester City).
Kuna pia Cedric Bakambu (DR Congo na Villareal), Yannick Bolasie (DRC na Everton), Sadio Mane (Senegal na Liverpool) na Kalidou Koulibaly (Senegal na Napoli).
Samatta ndiye anashikilia tuzo ya Mwanasoka Bora Anayecheza Afrika aliyotwaa Januari mwaka huu kufuatia kushinda taji la Ligi ya Mabingwa Afrika na TP Mazembe ya DRC mwaka jana na kuwa mfungaji bora wa michuano hiyo.
Previous
Next Post »