TAMBUA UGOJWA WA HOMA YA INI


Ahlan wasahlan  mpenzi msomaji wa makala hii ya afya yako ambako tunaangazia zaidi magonjwa mbalimbali, Na leo tunazungumzia  ugonjwa wa HEPATITIS wengi tunafahamu kama homa ya ini.na Makala hii hukujia kila siku kwa hiyo ni kusihi usiache kufatilia

Hepatitis ni ugonjwa unaoshambulia ini unaosababishwa na virusi vya Hepatitis B (HBV) ambapo kwa bahati mbaya licha ya kuwa hatari kuliko hata Ukimwi kutokana na wepesi wa maambukizo yake, ugonjwa huo haufahamiki kwa wengi. Taarifa za Shirika la Afya Duniani (WHO) zinaeleza kuwa, kirusi cha homa ya ini kinaweza kuishi nje ya mwili wa binadamu kwa siku 7 na kwa wakati huu, kirusi hiki kinaweza kusababisha maambukizi iwapo mtu hajapata chanjo ya kuuzuia. Kwa sababu hiyo watu wengi wamekuwa wakiugua maradhi ya homa ya ini bila kujua, hali ambayo hupelekea ini kuathirika taratibu.

Dakta Yuki Mark wa Hospitali ya Parktown North, Johanesburg, nchini Afrika Kusini anasema kuwa, homa ya ini aina ya B inaweza kuua kimyakimya bila kuonyesha dalili zozote. Dakta Yuri Mark anaeleza kwamba, huenda dalili zikaonekana waziwazi miaka mingi baada ya mtu kuambukizwa, na zinapoonekana, huenda tayari ini limenyauka au lina saratani na magonjwa hayo huua asilimia 25 ya watu walio na virusi vya HBV. Hepatitis A

Hepatitis A ni ugonjwa unaosababisha maambukizi katika ini ingawa si ya muda mrefu unaosababishwa na virusi vinavyoitwa Hepatitis A Virus (HAV). Kwa kawaida virusi vya ugonjwa huu hupatikana katika kinyesi cha mtu aliyeambukizwa na husambaa kwa kula chakula au maji yenye virusi vya ugonjwa huo. Inakadiriwa kuwa makumi ya mamilioni ya watu duniani huambukizwa ugonjwa huo kila mwaka duniani huku kipindi cha kuambukiza hadi kupona ugonjwa huo ni hadi miezi sita. Virusi vya HAV husababisha maambukizo makali na ya haraka katika ini lakini si ya muda mrefu wala ya kudumu, na karibu katika kesi zote za ugonjwa huu mwili huondoa virusi hivyo mwilini baada ya majuma au miezi michache. Maambukizo ya homa ya ini aina ya A ingawa si hatari lakini ni makubwa zaidi katika maeneo watu wasiyozingatia usafi, na kesi za ugonjwa huo hushuhudiwa kwa wingi hasa kwa watoto. Maambukizo ya ugonjwa huo hupungua katika sehemu ambazo watu wanazingatia matumizi ya maji safi na salama.

             Dalili za Hepatit

Dalili za mwanzo za ugonjwa wa Hepatitis  huweza kufanana na mafua na kwa kawaida hudumu kwa miezi isiyopungua miwili na baadhi ya watu huweza kuugua kwa muda wa miezi 6. Dalili zake ni uchovu, homa, kichefuchefu, kukosa hamu ya kula na homa ya nyongo ya manjano na kuonekana kiwango cha nyongo katika mkojo hali ambayo huufanya mkojo kuwa rangi nyeusi. Dalili nyingine ni kuharisha na kinyesi chenye rangi ya udongo.

          Matibabu yake

Hakuna matibabu maalumu ya ugonjwa wa Hepatitis  isipokuwa wale walioambukizwa hushauriwa kupumzika na kula lishe bora pamoja na kutokunywa pombe na kula vyakula vyenye mafuta mengi. Pia kujiepusha kula dawa ambazo haziwezi kuchujwa kwa urahisi na ini kama vile dawa ya kutuliza maumivu za acetaminophen, hadi daktari atakaposema kuwa ini limepona kabisa. Huenda mtu aliyeugua Hepatitis A asiambukizwe virusi hivyo tena katika maisha yake kwani mwili wake hujenga kinga lakini anaweza kuambukizwa aina nyingine ya maradhi ya virusi vinavyoshambulia ini. Chanjo inaweza kuzuia mtu asiambukizwe virusi vya HAV na tunaweza kujiepusha kuambukizwa ugonjwa huu kwa kudumisha usafi wa vyakula na mazingira yetu. Ugonjwa wa homa ya ini aina ya A kwa nadra sana huweza kusababisha ugonjwa wa muda mrefu wa ini.


Vipimo vya Homa ya Ini

Ili kujua kuwa mtu ana homa ya ini na wapo ameambukizwa ugonjwa huo karibuni au muda mrefu uliopita anapaswa kufanyiwa vipimo kadhaa:

Kwanza ni kipimo cha HBsAg. hiki ni kipimo cha kuainisha iwapo umeambukizwa virusi vya homa ya ini vya HBV na je, una uwezo wa kuwaambukiza watu wengine au la? Kipimo hiki huchunguza aina ya antigeni ambayo ni sehemu ya nje ya virusi na kupatikana kwake kwenye damu yako humaanisha kuwa una maambukizo ya u Hepatitis B yaliyo hai na unaweza kuwaambukiza wengine kwa urahisi.

Kipimo cha HBsAg kinapokuwa negative haina maana kuwa huna ugonjwa huo kwa asilimia 100, bali pengine virusi vimelala, uliambukizwa zaidi ya miezi 6 iliyopita au chanjo yako bado ni imara.

Kipimo cha pili cha Hepatitis B ni Anti-HBs. Kipimo hiki ni cha kuangalia iwapo mtu ana kinga ya virusi vinavyosababisha homa ya ini na iwapo mwili umetengeneza antigeni ya kupambana na ugonjwa huo. Kuwa positive kipimo hiki kunamaanisha hali mbili. Moja ni huenda ulipatiwa chanjo dhidi ya Hepatitis B, na hali ya pili ni kwamba huenda uliambukizwa ugonjwa wa homa ya ini humo nyuma. Katika hali zote mbili tulizozitaja iwapo kipimo cha Anti- HBs ni positive inamaanisha kuwa huwezi kuwambukiza wengine ugonjwa huo na pia virusi hivyo ingawa vipo mwilini mwako lakini vimelala na haviwezi kudhuru ini lako kwa kuwa, mwili una kinga inayotokana na mfumo wako wa kulinda mwili.

Kipimo cha tatu cha ugonjwa wa Hepatitis B ni Anti-HBc, ambacho huainisha iwapo uliwahi kuambukizwa ugonjwa huo huko nyuma au maambukizo ni ya hivi karibuni. Kipimo hiki huangalia antibodi inayotokana na sehemu ya ndani ya kirusi cha HBV inayopatikana kwa watu walioambukizwa ugonjwa huo. Iwapo kipimo hiki ni positive inamaanisha kuwa, kuna uwezekano una maambukizo ya muda mrefu ya homa ya ini yaliyo hai na unaweza kuwaambukiza wengine. Jawabu chanya la kipimo hiki pia huweza kumaanisha kwamba, uliambukizwa zaidi ya miezi 6 iliyopita lakini haupo katika hali ya hatari.

Vipimo vingine vya nyongeza ni HBeAg na Anti-HBe ambavyo huonesha kwa kiasi gani unaweza kuwaambukiza wengine ugonjwa huo na kiwango cha virusi vya homa ya ini mwilini. Vipimo vyote hivyo tulivyovitaja iwapo vitakuwa negative, basi inaamanisha huna ugonjwa wa Hepatitis B, na hivyo unapaswa kupata chanjo dhidi ya ugonjwa huo. Kwa wale ambao hawana ugonjwa wa ini bali walishawahi kupata chanjo dhidi ya ugonjwa huo, vipimo vyote tulivyotaja hapo juu huwa negative isipokuwa kipimo cha Anti-HBs.

Kwa wale wanaopatikana na maambukizo ya ugonjwa huo, vipimo zaidi hufanywa kama vile ultrasound ili kuonesha mabadiliko ya ini, kwani kama tulivyosema virusi vya Hepatitis huathiri seli za ini. Baadhi ya wakati pia MRI na CT scans hufanywa ili kuangalia uvimbe katika ini kwa watu ambao virusi vya ugonjwa huo tayari vimewasababishia vidonda katika ini au kitaalamu liver cirrhosis na pia kensa.

Kipimo kingine ni Alpha-foteprotein (AFP) kwa ajili ya kuangaliwa kiwango cha protein aina ya AFP inayotengenezwa na seli za ini zilizo na saratani. Kipimo hiki huonesha iwapo mgonjwa ana satarani ya ini au la.

Kipimo cha mwisho ni biopsy ya ini ambayo kwa ujumla huonesha uzima wa ini. Kipimo hiki hufanywa ili kupata uhakika iwapo ini lina vidonda au kensa.

Dawa yake:

Mtu ambaye ameambukizwa virusi vya Hepatiti  anapaswa kwenda kituo cha afya au kumuona daktari haraka. Kwa kawaida mwathirika hutakiwa kupata chanjo ya ugonjwa huo ndani ya masaa 24 baada ya virusi kuingia mwilini ambayo huenda ikazuia kujitokeza ugonjwa wa homa ya ini. Kwa wale ambao wamepatikana na maambukizo lakini sio ya muda mrefu kwa kawaida hakuna matibabu yoyote wanayopewa bali hupatiwa matibabu ya kupunguza dalili za ugonjwa huo wakati mwili ukipambana na virusi vya HBV.

Watu wengi hupona kabisa ugonjwa huo baada ya miezi kadhaa bila virusi kuharibu maini yao. Kwa kawaida hakuna matibabu ya homa ya ini ya muda mfupi isipokuwa wagonjwa hushauriwa kupima damu mara kwa mara hadi pale virusi vitakapoondoka mwilini. Lakini kwa wagonjwa wenye Hepatitis sugu ya muda mrefu, wanapaswa kuonana na daktari maalumu anayehusika na magonjwa ya ini ili wapate matibabu ya ugonjwa huo. Dawa zinazotolewa ili kutibu ugonjwa wa homa ya ini ni dawa za kupambana na virusi kwa ajili ya kuzuia vijidudu vya Hepatitis visiharibu ini na dawa hizo ni kama Entecavir, Interferon Alpha, Lamivudine, Tenofovir n.k. Dawa hizo hutolewa ili kupunguza kasi ya madhara ya virusi kwenye ini kwa kuzuia visizaliane zaidi na kusababisha vidonda au saratani ya ini. Mgonjwa anapaswa kupata ushauri wa daktari kabla ya kutumia dawa hizo. Lakini hata hivyo mgonjwa wa homa ya ini hata anayetumia dawa anaweza kuwaambukiza wengine. Kwa sababu hiyo jambo muhimu kwa wagonjwa wenye maambukizo ya Hepatitis  ni kufanyiwa vipimo vya damu mara kwa mara ili kujua matibabu yanavyokwenda na kujua iwapo kuna mabadiliko yoyote katika ini. Jambo jingine muhimu ni mgonjwa kupata maelekezo kutoka kwa wauguzi wa afya ili kuufahamu vyema ugonjwa wake na kuhakikisha kwamba hasambazi na kuwaambukiza watu wengine ugonjwa huo.

Kinga ya Homa ya Ini:

ugonjwa wa homa ya ini una kinga inayoweza kuzuia maambukizo ya virusi vya HBV. Ingawa kuna makundi maalumu ya watu wanaopaswa kupewa chanjo dhidi ya ugonjwa wa Hepatitis  lakini katika nchi nyingi duniani chanjo hiyo hutolewa kwa watoto pindi wanapozaliwa. Uchunguzi umeonesha kuwa, kuwapatia chanjo hii watoto pindi wanapozaliwa sio tu kumepunguza hatari ya maambukizo kwa kiasi kikubwa bali pia kumepunguza kesi za kensa ya ini. Watoto wote wanapaswa kupewa chanjo ya HBV wakiwa wachanga na kumalizia dozi ya ugonjwa huo wanapokuwa na miezi 18. Pia watoto na vijana hadi wa miaka 18 ambao hawakupatiwa chanjo hiyo walipokuwa wadogo wanapaswa pia kupatiwa. Watu wengine wanaopaswa kupatiwa chanjo ya homa ya ini mbali ma wale tuliowataja huko nyumba ni wanafamilia wanaoishi katika nyumba yenye mtu aliyeambukizwa virusi vya HV. Hii inamaanisha kuwa, kwa wagonjwa wenye Hepatitis , familia zao pia zinapaswa kupewa chanjo hiyo. Wengine ni wagonjwa wa HIV, wagonjwa wa kisukari walio na umri chini ya miaka 60, wafungwa na mahabusu, wanaofanyiwa dialysis, wenye magonjwa sugu ya ini, wanaosafiri kwenye nchi zenye maambukizo makubwa ya homa ya ini na wanaofanya kazi za kuwahudumia watu wasiojiweza.




Previous
Next Post »